Matthew 27:15-31

15 aBasi ilikuwa ni desturi ya mtawala kumfungua mfungwa mmoja aliyechaguliwa na umati wa watu wakati wa sikukuu. 16Wakati huo alikuwepo mfungwa mmoja mwenye sifa mbaya, aliyeitwa Baraba. 17 bHivyo umati wa watu walipokusanyika, Pilato akawauliza, “Mnataka niwafungulie nani, Baraba au Yesu yeye aitwaye Kristo?” 18 cKwa kuwa alitambua Yesu alikuwa amekabidhiwa kwake kwa ajili ya wivu.

19 dPilato akiwa ameketi kwenye kiti cha hukumu, mkewe akampelekea ujumbe huu: “Usiwe na jambo lolote juu ya mtu huyu asiye na hatia, kwa kuwa leo nimeteseka sana katika ndoto kwa sababu yake.”

20 eLakini viongozi wa makuhani na wazee wakaushawishi ule umati wa watu kwamba waombe Baraba afunguliwe, naye Yesu auawe.

21Mtawala akawauliza tena, “Ni yupi kati ya hawa wawili mnayetaka niwafungulie?”

Wakajibu, “Baraba.”

22 fPilato akawaambia, “Basi nifanye nini na huyu Yesu aitwaye Kristo?”

Wakajibu wote, “Msulubishe!”

23Pilato akauliza, “Kwa nini? Amefanya kosa gani?”

Lakini wao wakazidi kupiga kelele, wakisema, “Msulubishe!”

24 gPilato alipoona kwamba hawezi kufanya lolote, lakini badala yake ghasia zilikuwa zinaanza, akachukua maji, akanawa mikono yake mbele ya ule umati wa watu, akasema, “Sina hatia juu ya damu ya mtu huyu, hili ni jukumu lenu!”

25 hWatu wote wakajibu, “Damu yake na iwe juu yetu na juu ya watoto wetu!”

26 iBasi akawafungulia Baraba. Lakini baada ya kuamuru Yesu achapwe mijeledi, akamtoa ili asulubishwe.

Askari Wamdhihaki Yesu

(Marko 15:16-20; Yohana 19:2-3)

27 jKisha askari wa mtawala wakampeleka Yesu kwenye Praitorio
Praitorio maana yake ni makao makuu ya mtawala, jumba la kifalme lililokuwa linakaliwa na Pontio Pilato huko Yerusalemu, palipokuwa na kiti cha hukumu.
na wakakusanya kikosi kizima cha askari kumzunguka.
28 lWakamvua nguo zake na kumvika vazi la rangi nyekundu, kisha 29 mwakasokota taji ya miiba, wakaiweka kichwani pake. Wakamwekea fimbo katika mkono wake wa kuume, na wakapiga magoti mbele zake na kumdhihaki, wakisema, “Salamu, mfalme wa Wayahudi!” 30 nWakamtemea mate, wakachukua ile fimbo wakampiga kichwani tena na tena. 31 oBaada ya kumdhihaki, wakamvua lile joho, wakamvika tena nguo zake. Kisha wakampeleka ili wakamsulubishe.

Copyright information for SwhNEN